Home » » Watakiwa kutekeleza imani ya CCM

Watakiwa kutekeleza imani ya CCM

VIONGOZI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wakiwamo Wabunge, Wawakilishi pamoja na Madiwani, wametakiwa kutekeleza Ilani ya CCM ili kuhakikisha CCM inashinda katika uchaguzi ujao.
Hayo yalisemwa na Katibu wa Kamati Maalumu ya CCM, Idara ya Itikadi na Uenezi ya CCM Zanzibar, Waride Bakari Jabu, wakati akizungumza na wanachama wa chama hicho huko Bumbwini Misufini, katika mkoa wa Kaskazini B, Unguja.
Jabu alisema, CCM imechaguliwa na wananchi kushika nafasi ya kuongoza serikali ambapo hatua hiyo inaonesha wazi kwamba wananchi wameridhika na kujenga imani dhidi ya chama hicho kwa ajili ya kuwaletea maendeleo.
Alisema viongozi hawana budi kutekeleza Ilani ya chama ya mwaka 2016-2020, pamoja na ahadi za viongozi hao walizotoa katika majimbo ya uchaguzi.
“Chama Cha Mapinduzi kimepewa ridhaa ya kuongoza nchi katika uchaguzi wa mwaka jana, ambapo viongozi wajibu wao mkubwa, ni kutekeleza kwa vitendo ilani pamoja na ahadi zote walizotoa kwa wananchi na wanachama,” alisema.
Jabu alisema kwa kiasi kikubwa CCM, imeridhishwa na juhudi zinazochukuliwa na viongozi wa majimbo ya uchaguzi katika kutekeleza na kusimamia miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa miradi ya maji safi na salama na ujenzi wa shule za msingi.
Awali, Katibu wa Idara ya Oganaizesheni ya CCM, Haji Mkema, amewataka wanachama kuimarisha chama kwa kulipia kadi za uanachama kwa wakati pamoja na kupeperusha bendera za chama katika matawi ya CCM.
Alisema kulipia kadi kwa wakati ndio uhai wa CCM katika majimbo ya uchaguzi ambao utasaidia kuongeza ari kwa wananchi wa kawaida kujiunga na chama hicho.
“Viongozi wa CCM fanyeni kazi ya kuhamasisha wanachama kulipa ada za uanachama kwa wakati pamoja na kuweka bendera za chama katika matawi au sehemu za mabalozi,” alisema.
Mkema aliwahakikishia wanachama kwamba uchaguzi umekwisha na utafanyika mwingine ifikapo 2020 na kazi kubwa iliyopo ni kuimarisha chama ikiwemo kuingiza wanachama wapya kupitia katika jumuiya za chama.

CHANZO GAZETI LAHABARI LEO

0 comments:

Post a Comment

 
Support by Tone multimedia company Limited
Copyright © 2012. Zanzibar Yetu - All Rights Reserved
Designed by by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa